AMEFUNGUKA kwa mara ya kwanza! Baada ya kusambaa kwa maneno ya
chinichini kwamba mkali wa Bongo Fleva, Nasibu Abdul ‘Diamond Platnumz’
amemuangukia mzazi mwenzake, Zarinah Hassan ‘Zari The Boss Lady’
akimuomba radhi ili warudiane, staa huyo ameibuka na kutolea ufafanuzi
ishu hiyo.
Ubuyu huo uliosambaa kwa kasi kwenye mitandao ya kijamii, uliibuka hivi
karibuni na kueleza kuwa, kwa nyakati tofauti, Diamond alitinga nchini
Afrika Kusini ‘Sauz’, nyumbani kwa mwanamama huyo wa Kiganda na kumuomba
msamaha ili waweze kurudiana na kulea watoto wao wawili, Tiffah na
Nillan.
ETI NI KWA SABABU KAMKOSEA…
Ubuyu huo ulikolezwa nakshi mitandaoni baada ya kuaminika kuwa, Diamond
ndiye mwenye makosa ndiyo maana Zari alitangaza kumuacha.
KWA NINI ZARI ALIMUACHA?
Mara kadhaa Zari amekuwa akieleza wazi kwamba, kilichomsababisha aamue
kummwaga Diamond ni kutokana na kutokuwa mwaminifu na kuhisi anamkosea
heshima.
MAHOJIANO ‘KARENTI’
Kwenye mahojiano yake ya hivi karibuni ‘karenti’ jijini Nairobi, Kenya,
Zari alisema kuwa, aliamua kumpiga chini Diamond kutokana na matendo
yake maovu (michepuko) na kamwe hayuko tayari kurudiana naye.Alisema
kuwa, ataendelea kubaki kuwa baba wa watoto wake, lakini uhusiano wao
hauwezi kufufuka upya kwa sababu ya usalama wake.
TUANGAZIE VYANZO VINGINE
Vyanzo vingine ambavyo vilizungumza na Ijumaa Wikienda viliushibisha
zaidi ubuyu wa mkali huyu wa ngoma ya African Beauty kwa kueleza kuwa,
Diamond anahaha kunusuru uhusiano wake kwani Zari ndiye mwanamke pekee,
chaguo la mama yake, Sanura Kassim ‘Sandra’.
“Hakuwa na jinsi, mama yake hamtaki Mobeto (Hamisa) kama ulivyoona
juzikati alimpa vitasa. Mama Diamond kipenzi chake ni Zari hivyo hiyo
pia imechangia kumshawishi Diamond aende Sauz kuomba radhi,” kilieleza
chanzo kimoja, madai ambayo pia yalielezwa na vyanzo vingine tofauti.
KWA NINI
DIAMOND ANASEMAJE?
Baada ya kupata ubuyu huo kutoka vyanzo mbalimbali, wikiendi iliyopita
Ijumaa Wikienda lilimtafuta Diamond ambapo kwa mara ya kwanza tangu
aachwe na Zari alimzungumzia mrembo huyo aliyempa heshima ya kuwa baba
kwa kumzalia watoto hao wawili kwani kabla ya hapo alisimangwa kutokana
na ishu ya kutopata mtoto na msururu wa warembo ‘aliodozi’ nao
kimalovee.
AKATAA KUZUNGUMZIA YA KENYA
Kwenye mazungumzo hayo maalum, Diamond alikataa kuzungumzia kauli za
Zari alizozitoa hivi karibuni huko Nairobi dhidi yake kwa kile alichodai
kuwa hakina maana kwa sasa. “Hayo ya Kenya bwana achana nayo maana
yameshapita, mimi nafikiri niulize kuhusu haya ya sasa itapendeza,”
alisema Diamond.
KUHUSU KUOMBA RADHI SASA…
Alipoulizwa kuhusu madai hayo mapya ya kudaiwa kuenda Sauz mara kadhaa
kumuomba radhi mama watoto wake huyo, Diamond alianza kwa kukiri kwenda
nyumbani kwa Zari, Sauz kisha akafafanua zaidi madai hayo.
“Ni kweli ninaenda. Siyo mara moja au mara mbili nimeenda. Nakwenda kule
si kwa maana ya kumuomba msamaha, hapana. Nakwenda kule kwa ajili ya
kuwaona wanangu. “Haiwezekani eti niwe natuma tu fedha kwa ajili ya
matumizi halafu nimeenda Sauz, nisiende kuwaona wanangu, hilo litakuwa
ni jambo la ajabu sana.
“Hao wanaosema kwamba sijui nimemuangukia, nafikiri itakuwa ni maoni yao
tu na stori za kutunga, lakini kimsingi ni kwamba hayana ukweli wowote.
“Zari ni mama wa watoto wangu na itabaki kuwa hivyo,” alisema Diamond.
TUMEFIKAJE HAPA
Baada ya kuugulia moyoni kwa muda mrefu, Februari 14, mwaka huu, Zari
‘yalimfika hapa’, akaona isiwe tabu, kupitia ukurasa wake wa Instagram,
akatangaza rasmi kummwaga Diamond.
Badala ya kuposti maua yenye kuashiria upendo kwa maana ya kusherehekea
sikukuu ya Wapendanao (Valentine’s Day), Zari aliposti ua jeusi na
kusindikiza na ujumbe mzito uliobeba hoja za kwa nini ameamua
‘kumtapika’ Diamond.
UJUMBE ULISOMEKA WENYEWE
Kwenye ujumbe huo, Zari, mama wa watoto watano, alisema anatambua kwamba
ilikuwa vigumu kwake kufikia umauzi huo, lakini hakuna namna anayoweza
kufanya kulinda heshima yake kwani Diamond amekuwa akihusishwa na skendo
mbalimbali za wanawake katika vyombo vya habari. Mwisho akapigilia
msumari ujumbe wake kwa kusema ameamua kuachana na Diamond kama mpenzi
wake, lakini ataendelea kubaki kama baba wa watoto wake.
WANAWAKE WENYEWE NI WAPI?
Licha ya kwamba yapo maovu ambayo yanadaiwa kufanywa kwa siri na
Diamond, lakini yaliyoweza kunaswa na mapaparazi na kupamba vyombo vya
habari ni pamoja na ishu ya kumpa mimba mwanamitindo Hamisa Mobeto.
Huku akiwa kwenye uhusiano mzito na Zari, Diamond alijiiba kwa siri na
kufanikiwa ‘kummega kisela’ Mobeto hadi kuzaa naye mtoto mmoja, hali
ambayo inadaiwa kumkasirisha mno Zari. Kama hiyo haitoshi, imedaiwa kuwa
madai ya Diamond kurudiana na mrembo Wema Isaac Sepetu nayo yalikuwa
yakimkosesha usingizi Zari.
Stori: Mwandishi Wetu, Dar